09/07/2026
VETA
This is an official account for the Vocational Education and Training Authority (VETA).
09/07/2026
09/07/2026
'SAMANI ZETU ZINA KIWANGO CHA KIMATAIFA' WATANZANIA WATHAMINI VYA KWAO-VETA. Chuo cha Ufundi stadi VETA kimekuwa kivutio kikubwa katika maonesho...
08/07/2026
VETA Yaanza Mafunzo ya Uchimbaji Madini Chini ya Ardhi, Wataalamu Wazawa Kuongezeka
Tanzania inatarajia kuongeza idadi ya wataalamu wazawa wenye ujuzi wa kisasa katika sekta ya madini baada ya Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kuzindua mitaala sita ya mafunzo ya uchimbaji wa madini chini ya ardhi, hatua inayolenga kuimarisha ushiriki wa Watanzania katika miradi ya madini na kuchangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Akizungumza Julai 8, 2026 wakati wa kupokea rasmi mitaala hiyo na mpango wa utekelezaji wake, Mwenyekiti wa Chemba ya Migodi Tanzania (TCM), Mhandisi Philbert Rweyemamu, amesema sekta ya madini inaendelea kuwa mhimili muhimu wa ukuaji wa uchumi kupitia uzalishaji, ajira, mapato ya Serikali na maendeleo ya viwanda, hivyo inahitaji nguvu kazi yenye ujuzi unaokidhi matumizi ya teknolojia za kisasa katika uchimbaji wa madini chini ya ardhi.
Amesema kwa miaka mingi kampuni za madini zililazimika kuajiri wataalamu kutoka nje ya nchi kutokana na uhaba wa wataalamu wa Kitanzania, lakini kupitia Mradi wa Mafunzo ya Ufundi wa Madini (IMTT), VETA imeanza kuzalisha wahitimu wenye uwezo wa kufanya kazi katika migodi ya ndani na nje ya nchi.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Mkurugenzi wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Dkt. Abdallah Ngodu, amesema mitaala hiyo imeandaliwa kwa ushirikiano wa VETA na wadau wa sekta pamoja na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET), ili kuhakikisha wahitimu wanapata ujuzi unaohitajika katika soko la ajira.
Amesema, kwa hatua ya awali, utekelezaji wa mitaala hiyo utaanza katika Chuo cha Ufundi Stadi na Huduma Moshi.
Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Chemba ya Migodi Tanzania, Mhandisi Benjamin Mchwampaka, amesema kuanza kutumika kwa mitaala hiyo kutaimarisha utekelezaji wa sera ya ushiriki wa Watanzania katika sekta ya madini (Local Content) kwa kuzalisha wataalamu wazawa watakaopunguza utegemezi wa wataalamu kutoka nje ya nchi.
Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Kaskazini, Monica Mbelle, ameeleza kuwa mitaala hiyo inahusisha mafunzo ya Uendeshaji wa Mitambo ya Kubeba na Kusafirisha Miamba Migodini; Uendeshaji wa Mitambo ya Kuchimba Mahandaki; Uendeshaji wa Mitambo ya Kuchimba Mashimo Marefu; Uendeshaji wa Mitambo ya Kuchimba Mashimo ya Ndani ya Miamba; Maandalizi ya Ulipuaji wa Miamba Chini ya Ardhi pamoja na Matumizi Salama ya Vifaa vya Kunyanyua na Kufunga Mizigo.
07/07/2026
VETA Tunawatakia maadhimisho mema ya Sikukuu ya Sabasaba.
06/07/2026
KATIBU MTENDAJI NACTVET APONGEZA USHIRIKIANO WA VETA NA VIWANDA
Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET), Dkt. Mwajuma Lingwanda ameipongeza Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kwa kukuza ushirikiano na viwanda na waajiri katika utoaji wa elimu na mafunzo ya ufundi stadi.
Dkt. Lingwanda ametoa pongezi hizo alipotembelea banda la VETA, kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa Dar es Salaam, leo tarehe 6 Julai 2026 na kushuhudia wadau mbalimbali wanaoshirikiana na VETA katika utoaji mafunzo.
Akiwa kwenye kizimba cha wadau wa VETA ndani ya banda hilo, Dkt. Lingwanda alitolea mfano wa ushirikiano wa VETA na Kampuni ya Emirate Aluminum Profile kuwa ni mfano wa kuigwa na waajiri na wenye viwanda wengine.
Sambamba na hilo, Dkt. Lingwanda alipongeza juhudi mbalimbali zinayofanywa na VETA katika kukuza ubora wa mafunzo ikiwemo mafunzo yanayolenga kutoa tunuku za kimataifa; uendelezaji ubunifu na uzalishaji katika vyuo vyake.
VETA inashiriki katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa Dar es Salaam (Sabasaba) yakiwa na kaulimbiu ya _Maonesho ya Biashara ya Kimataifa, Sabasaba, Fahari ya Tanzania._
06/07/2026
Balozi wa Tanzania China aahidi kuiunganisha VETA na taasisi za Kichina
Balozi wa Tanzania nchini China, Dkt. Suleiman Haji Suleiman ameiomba Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kuandaa na kuwasilisha kwake maandiko ya kimkakati kuhusu mwelekeo wake katika utoaji mafunzo na uendelezaji ujuzi ili aweze kusaidia kutafuta fursa za ushirikiano na taasisi za nchini China katika teknolojia na utoaji mafunzo.
Balozi Suleimani ametoa wito huo leo, tarehe 6 Julai 2026 alipokutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), CPA Anthony Kasore, katika banda la Ubalozi huo kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa, Dar es Salaam (Sabasaba).
Amesema, anatamani kuiona VETA inaongeza zaidi ubora wa mafunzo na kuzalisha wahitimu mahiri wenye uwezo wa kiteknolojia.
Amesema ameona fursa nyingi za kiteknolojia nchini China ambapo kukiwa na ushirikiano wa karibu wa VETA na taasisi mbalimbali za China, kunaweza kuwa na fursa za ujengeaji uwezo wakufunzi wa VETA na ubadilishanaji maarifa na uzoefu katika nyanja mbalimbali.
Amesema, anatarajia kupanga ziara ya kimafunzo (study tour) kwa ajili ya uongozi wa VETA katika viwanda na taasisi mbalimbali za China ili kuwezesha kupata uelewa mpana na kutambua fursa muhimu za ushirikiano.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA Anthony Kasore, amemshukuru Balozi Suleiman kwa kuonesha nia ya kuisaidia VETA kuboresha utoaji wa mafunzo na ukuzaji ujuzi na teknolojia kwa Watanzania.
Amesema, VETA itaufanyia kazi ushauri na maelekezo yake ili malengo yaweze kufikiwa.
05/07/2026
WANUFAIKA WA MRADI WA DUMISHA AMANI WAHAMASISHWA KUANZISHA VIKUNDI
Mkuu wa wilaya ya Lindi Mhe. Victoria Mwanziva amewataka wanafunzi 60 watakaonufaika na mafunzo ya ufundi kupitia ‘Mradi wa Dumisha Amani’ unaofadhiliwa na mashirika ya kimataifa ya UNPDF, UNDP-Tanzania na kampuni ya CPP kuunda vikundi vya stadi zoa ili iwe rahisi kwa Serikali kuweza kuwapatia mikopo.
Mwanziva amaetoa maagizo hayo tarehe 4 Julai, 2026 wakati wa hafla fupi ya ufunguzi rasmi wa mafunzo hayo katika Chuo cha Ufundi Stadi na Huduma cha Mkoa wa Lindi.
“Tuna vikundi vya vijana, vikundi vya maendeleo, karibuni sana Halmshauri tuna mikopo ya manispaa na ile ya asilimia 10 ya vijana, wanawake, wazee na wenye mahitaji maalum. Mikopo hii mtaipata mkiwa kwenye vikundi, ni rahisi kwani tayari mtakuwa na ujuzi na mkiwa na mpango unaotekelezeka mtaweza kunufaika na mikopo hii moja kwa moja,”amesema Mwanziva.
Mwanziva amewapongeza VETA, UNDPF, CPP, UNDP GPF-Tanzania kwa kuwezesha vijana kupata ujuzi kwa vitendo, stadi za maisha, ujasiriamali ili waweze kujiajiri au kujiriwa na kujikwamua kiuchumi.
Kwa upande wake Afisa Mkuza Mitaala Mwandamizi kutoka VETA Makao Makuu, Alphoncina James Mshana amesema nafasi waliyoipata vijana hao ni ya kipekee na yenye thamani kubwa, hivyo amewahimiza kuitumia kikamilifu kwa kuhudhuria mafunzo yote, kuzingatia nidhamu, kufuata maelekezo ya wakufunzi na kushirikiana vizuri katika kipindi chote cha mafunzo.
Naye Josphine Sepeku, Afisa Mradi wa Dumisha Amani kutoka UNDP-Tanzania amesema wataendelea kusaidia vijana wa Tanzania kupata mafunzo ambayo yanawapa stadi na maarifa ya kujitegemea, hivyo kuchangia katika kudumisha amani.
Aidha Mkuu wa chuo hicho, Harry Mmari amesema wanafunzi hao watapatiwa mafunzo ya vitendo katika stadi za Ufundi Umeme; Mapishi na Huduma za Hoteli; Ubunifu Ushonaji na Teknolojia ya Nguo; pamoja na Ufundi Bomba na hivyo ujuzi watakaoupata utakuwa mtaji muhimu wa maisha yao na msingi wa kujiletea maendeleo binafsi, ya familia zao na ya Taifa kwa ujumla.
Click here to claim your Sponsored Listing.
Location
Telephone
Website
Address
VETA Head Office, 12 VETA Road, 41104 Tambukareli, P. O. Box 802, Dodoma Tanzania, Email: Info@veta. Go. Tz Telephone: +255 26 2963661 Fax: +255 22 2863408 Url: Www. Veta. Go. Tz
Dodoma
PLOTNO.18
Opening Hours
| Monday | 07:30 - 21:30 |
| Tuesday | 08:00 - 21:30 |
| Wednesday | 07:30 - 21:30 |
| Thursday | 07:30 - 21:30 |
| Friday | 07:30 - 21:30 |
09/07/2026
09/07/2026