Simulizi za ALLY H.

Simulizi za ALLY H.

Share

Huu ni uwanja unahusu simulizi za maisha zenye kuburudisha na kuelimisha lakini zenye kuzingatia maa

21/06/2026

SIMULIZI: NAHITAJI NIMFAHAMU
​Mtunzi: Ally H.

SEHEMU YA 10

Nilikaa ukingoni mwa kitanda changu kwa masaa kadhaa, macho yangu yakiwa yameganda kwenye kioo cha simu iliyokuwa mkononi mwangu. Ule ujumbe mfupi ulikuwa k**a fumbo zito lililotupa nanga akilini mwangu.

​Kwa kawaida, mimi si mtu wa kuamini mambo kirahisi. Maisha yamenichanja chale nyingi za siri, yamenifundisha kuwa kila jambo lina mzizi wake, na kila kivuli unachokiona kina chanzo cha mwanga mahali fulani. Lakini usiku ule, kadri nilivyojaribu kuiliwaza nafsi yangu, ndivyo mapigo ya moyo wangu yalivyozidi kwenda kasi, yakigonga ukuta wa kifua changu kwa fujo.
​Nikaufungua tena ule ujumbe, kana kwamba maneno yake yangebadilika.

​"Ukifika kwa Mzee Ling’ande… muulize kwanini hakukuambia ukweli wote."

​Mwishoni mwa ujumbe huo, kulikuwa na herufi moja tu iliyosimama k**a alama ya kiada.
Z.

​Nilizima kioo cha simu. Giza likatanda chumbani, lakini giza kubwa zaidi lilikuwa moyoni mwangu.

​Nilinyanyua mkono wangu wa kushoto na kuitazama ile pete. Ilikuwa bado imeng'ang'ania kidoleni mwangu. Lakini haikuwa tena ile pete ya ajabu niliyokusudia kuivua hapo mwanzo. Jiwe lake lililokuwa likimeta sasa lilikuwa limepoteza nuru na kudhoofu.

​Hata hivyo, yale maandishi ya siri yaliyokuwa yamechongwa kwa ndani yalikataa kufutika akilini mwangu.

“USIFIKIRI SAFARI IMEISHA.”

​Nikainamisha kichwa, nikishika paji langu la uso. K**a kuna kitu kilikuwa kinanitesa usiku ule, haikuwa ile meseji yenyewe. Ilikuwa ni ukweli mchungu kwamba… nilikuwa tayari nimejiaminisha kuwa kila kitu kimefika tamati.

Niliamini dhoruba imetulia. Nimempata Zuwena, mwanamke ambaye angeweza kuyaponya majeraha yangu na kunifanya niamini tena katika upendo. Niliamini pete ilikuwa imetimiza jukumu lake la siri.

​Sasa, huu "ukweli wote" unaozungumziwa hapa ulikuwa ni ukweli gani? Je, nilikuwa ninaishi kwenye kivuli cha uongo?

​Nilijaribu kuipiga ile namba iliyotuma ujumbe ule. Sauti ya mwanamke wa mtandao ikajibu kwa ubaridi.

"Nambari unayopiga haipatikani kwa sasa..."

Nikajaribu tena na tena. Lakini sikufanikiwa.
Kwa vidole vilivyokuwa vikitetemeka kidogo, nikaandika ujumbe wa maandishi

"Wewe ni nani? Na unataka nini kwangu?"

​Nikasubiri.
Dakika ya kwanza ikapita…
Ya pili…
Ya tano…
Kimya kikuu kilitawala. Hakuna jibu.

​Usiku ule ulikuwa mrefu na wa mateso. Usingizi ukawa bidhaa adimu kwangu, ukajificha mbali na kope zangu. Kila nilipofumba macho, niliona sura ya Mzee Ling’ande na swali moja lililokuwa likivuma k**a mwangwi milimani. Mzee Ling’ande alikuwa ameficha siri gani kubwa kiasi hicho?

​Asubuhi ilipofika, nilijivuta kitandani mapema huku macho yakiwa yamefanya maduara meusi kwa kukosa usingizi. Nilijimwagia maji ya baridi ili kuamsha akili yangu, nikavaa nguo zangu haraka kujiandaa na safari ya kwenda Lindi.

​Baada ya kuhakikisha maandalizi yamekamilika. ​Nilitoka nje, upepo mwanana wa asubuhi ukanipokea. Lakini kabla sijaelekea kituo cha mabasi kuanza safari yangu, moyo wangu ulisikitika na kunivuta upande mwingine. Moyo wangu ulikuwa na kiu ya kumuona Zuwena kabla sijaondoka. Nilihitaji nishati ya tabasamu lake ili nistahimili safari yangu.

​Niliingia hospitalini kukiwa na pilikapilika za kawaida za asubuhi. Harufu ya dawa, sauti za chini za wagonjwa na vishindo vya viatu vya madaktari vilitawala korido.

Nilimwona Zuwena kwa mbali. Alikuwa ameketi mapokezi, ameinamisha kichwa chake kwa umakini huku akijaza taarifa kwenye faili kubwa la wagonjwa.

​Sikumwita. Nilibaki nimesimama hatua chache kutoka kwake, nikivinjari uzuri wake na utulivu uliokuwa unamzunguka. Alikuwa k**a chemchemi ya maji katikati ya jangwa la mawazo yangu.

​Baada ya sekunde kadhaa, kana kwamba alihisi uwepo wa mtu anayemkodolea macho, alinyanyua uso wake. Macho yetu yalipokutana, uso wake uling'aa mara moja na tabasamu pana likachanua midomoni mwake.

"Clever?" alitamka jina langu kwa sauti iliyosikika k**a muziki mtamu masikioni mwangu.

​Nikamsogelea na kuegemea kaunta. "Habari ya asubuhi, daktari wangu."
"Nzuri sana. Kumbe bado hujasahau njia ya kuja hospitali?" alitania, huku akicheka kidogo.

Nikacheka pia. "Nilikuwa napita tu hapa karibu." Akakunja midomo yake kwa namna ya kuvutia. "Unasema unapita tu, lakini umesimama hapo ukinikagua kwa dakika kadhaa bila kusema kitu. Hiyo nayo inaitwa kupita?"

​Nikaona sina ujanja, nikavuta kiti kilichokuwa karibu na kuketi. Akaendelea kuandika kitu kwenye faili lile kwa sekunde chache, kisha akalifunga na kugeuka mzima mzima kunitazama. Macho yake yakatua kwenye uso wangu, na kwa ghafla, uchangamfu wake ukapungua, ukabadilika na kuwa wa huruma na umakini.

"Leo upo kimya sana, Clever. Kuna nini?"

Nikatikisa kichwa, nikijaribu kuvaa tabasamu la bandia. "Hakuna kitu, ni kawaida yangu tu."

Akacheka kicheko kifupi cha kutokuamini. "Hapana, si kweli."
Nikamwangalia machoni.

​Akaniambia maneno yaliyochoma hisia zangu.
"Wewe ukijifanya uko sawa, huwa unasahau kuwa macho yako huwa yanatoa siri yote. Yanasikitika."

Nilishindwa kuhimili macho yale, nikacheka kwa unyonge. "Ah, kweli? Unaanza kunisoma sasa hivi?"

Zuwena alivuta pumzi ndefu, kisha akashusha mabega yake. "Sijui..."

Akatulia kidogo, kisha akasema huku
akinitazama kwa macho yaliyojaa hisia za dhati: "Labda nimeanza kukuzoea sana, Clever."

​Nilihisi joto la ghafla likisambaa kifuani mwangu. Tabasamu la kweli lililochochewa na maneno yake likanijia lenyewe. Ili kuficha jinsi nilivyoguswa, nikageuza uso wangu upande wa pili na kumuuliza kwa sauti ya chini.

"Na k**a nikikwambia kwamba nina safari?"

Macho yake yakapanuka kidogo.

"Unaenda wapi?"

"Lindi," nilimjibu kifupi.

​Zuwena alibaki kimya. Haikuwa ile hali ya kushangaa ghafla, bali ilikuwa k**a mtu ambaye jina hilo la mahali limeamsha mawazo fulani mazito kichwani mwake.

Baada ya sekunde chache, alitamka taratibu: "Lindi..."

Nikamtazama, nikitaka kusoma nini kiko nyuma ya mtazamo wake. Kuna wakati yalinijia mawazo nitoe simu nimuoneshe ule ujumbe kwenye simu yangu, ile herufi Z ilinifanya niwaze isije kuwa ni yeye Zuwena. Kilichonifanya niwaze hayo ni yale mabadiriko niliyoyaona baada ya kumwambia kuhusu safari yangu ya Lindi, akili yangu ilinikataza nisifanye hivo.

Zuwena alitabasamu tena, lakini safari hii tabasamu lake lilikuwa na chembe ya upweke.

"Sijui kwanini… ila umesema unaenda Lindi, na kwa ghafla nimehisi hii si safari ya kawaida ya kikazi au mapumziko. Kuna kitu kikubwa unachoenda kukifuata."

​Nikalazimisha kicheko. "Sasa mbali na utatuzi wa matatizo ya hospitali, umekuwa mtabiri wa safari pia?"

Akacheka kwa sauti ya chini, sauti iliyotulia. "Hapana, mimi si mtabiri."
Akatulia tena, kisha akasema kwa sauti iliyojaa upole uliopenya hadi mifupani mwangu: "Ila… nakuomba usikae sana huko."

Nilimtazama na kumuuliza kwa shauku, "Kwa nini?"

​Zuwena aliepuka macho yangu haraka, akajifanya bize kupanga mafaili yaliyokuwa mezani kwake ili kuficha aibu. Kisha akasema kwa sauti ya kunong'ona.

"Kwa sababu..." akatabasamu kwa aibu na kuendelea, "Kuna watu ambao ukishazoea uwepo wao karibu yako… wakiondoka hata kwa siku chache, unaanza kuhisi kuna nafasi kubwa iko wazi. Unaanza kuwamisi"

​Nilimkodolea macho, nikizama kabisa kwenye uzuri wa maneno yake.

Aligundua kuwa nimemkazia macho, uso wake ukabadilika rangi kuwa mwekundu kwa aibu, akatazama pembeni haraka sana na kuongeza: "Namaanisha… watu wa nyumbani kwako, mama yako na ndugu zako."

Nikacheka kwa furaha ambayo sikuwa nayo asubuhi yote. "Na wewe je? Utanimisi?"

Akanitazama kwa sekunde mbili, macho yetu yakifanya mazungumzo ya siri ambayo midomo isingeweza kuyasema. Halafu akatabasamu kwa madoido. "Usijisifu sana, Clever. Nenda bwana!"

​Tulicheka wote wawili, na lile vazi la huzuni lililokuwa limenitanda likaanza kupungua uzito.

Nilinyanyuka kwenye kiti ili kuondoka. Lakini kabla sijapiga hatua ya tatu kuelekea mlangoni… sauti yake iliniita tena, safari hii ikiwa na uzito wa kipekee. "Clever."

Nikageuka na kumtazama.
​Alikuwa amesimama, akinitazama kwa utulivu na umakini mkubwa uliorudisha lile fumbo la usiku uliopita. Kisha akasema.
"Ukirudi… nitafurahi sana kusikia k**a ulifanikiwa kupata kile ulichoenda kukitafuta."

​Nilimkodolea macho kwa sekunde kadhaa, nikijaribu kutafakari maana ya kauli yake. Je, alijua kitu kuhusu safari hii? Nilishindwa kupata jibu, nikatikisa kichwa changu tu. "Sawa, Zuwena." Nikageuka na kuondoka.

​Nilipotoka nje ya milango ya hospitali, nilihisi upepo ukipita kwenye nywele zangu na nikajikuta natabasamu peke yangu k**a mwehu. Kwa mara ya kwanza baada ya miaka mingi ya upweke na maumivu… nilihisi kuna nafsi ya mtu inayonisubiri nirudi kwa hamu. Hiyo ilitosha kunipa nguvu.

​Mchana ulipofika, nilikuwa tayari ndani ya basi nikiwa safarini kuelekea Lindi. Ilikuwa ni barabara ile ile niliyopita miezi michache iliyopita. Miti ile ile iliyosimama kando ya barabara, vumbi lile lile.

​Mara ya kwanza nilienda Lindi nikiwa kijana aliyevunjika moyo, nikitafuta mwanamke wa kunipenda kwa dhati.

Lakini safari hiyo ya pili. Nilikuwa nimebeba kiu ya kupata ukweli uliokuwa umejificha kwenye giza.

Nilifika jioni sana, sikuweza kwenda moja kwa moja kwa mzee Ling'ande kwani kijiji alipokuwa ni mbali kufika na kuna wakati kunahitajika kupanda usafiri wa boda boda, hivyo ilibidi nisubiri siku iliyofuata.

Mapema siku iliyofuata niliweza kuwasili kwenye eneo alipokuwa akipatika mzee huyo. Nilianza kutembea kwa haraka kuelekea kwenye kijumba kidogo cha udongo cha Mzee Ling’ande.

Eneo lilikuwa tulivu, hakukuwa na watu k**a nilivyokuja mara ya kwanza, ​Nilipofika kwenye mlango wa nyumba yake… miguu yangu ilikak**aa na kusimama yenyewe, kana kwamba imepigwa shoti ya umeme.

​Nyumba ilikuwa imefungwa. Hakukuwa na moshi uliokuwa ukitoka jikoni k**a ilivyokuwa desturi yake. Hakukuwa na harufu ya mitishamba wala dalili yoyote ya kiumbe hai. Kila kitu kilionekana kutelekezwa. Kufuli kubwa la kizamani, lililoshika kutu, lilikuwa limening'inia mlangoni k**a ishara ya kifo cha matumaini yangu.

​Nilisimama hapo, nikiwa nimepigwa na bumbuazi, macho yangu yakitamaani kuona hata kivuli cha yule mzee.

​Mzee mmoja aliyekuwa anapita njia, akiwa amebeba jembe begani, alisimama na kunitazama kwa huruma.

Sura yangu ya kigeni na mshtuko uliokuwa usoni mwangu ulimfanya anisogelee.
"Kijana, unamtafuta nani mahali hapa?" sauti yake ilikuwa ya kizee na yenye mikwaruzo.

​Nikageuka kumtazama, sauti yangu ikitoka kwa tabu. "Namtafuta… Mzee Ling’ande. Mwenye nyumba hii."

​Yule mzee alinitazama kwa muda mrefu, macho yake yakibeba ujumbe mzito wa majonzi kabla hata hajayatoa mdomoni mwake. Akavuta pumzi ndefu ya majonzi, kisha akasema kwa sauti ya chini iliyozama masikioni mwangu k**a bomu.

"Kijana wangu… umesikitisha. Umechelewa sana."

​Kifua changu kilikaza, nikakunja uso kwa hofu. "Kivipi, mzee wangu?"

​Yule mzee alitikisa kichwa chake kwa masikitiko, akatazama ile nyumba iliyofungwa, kisha ak**aliza matumaini yangu yote yaliyosalia.

"Mzee Ling’ande hatunaye tena. Alifariki dunia mwezi mmoja uliopita."

​Nilihisi k**a dunia imesimama kuzunguka. Kitu kizito na chenye baridi kali kilipita kifuani mwangu, kikininyima uwezo wa kuvuta pumzi.

Macho yangu yalileta ukungu nikiiangalia ile nyumba iliyobeba siri ya maisha yangu.

​Niliuliza tena, kwa sauti ya tetemeko na ya chini kabisa, kana kwamba majibu yangekuwa tofauti.

"Unasema… mwezi mmoja uliopita?"

​Usikose Sehemu ya 11...

Karibu kwa maoni na ushauri.......

19/06/2026

SIMULIZI; NAHITAJI NIMFAHAMU
MTUNZI; ALLY H.

SEHEMU YA 09.

Baada ya kutoka hospitalini siku ile, nilimpeleka Zuwena nyumbani kwao k**a tulivyokubaliana. Safari yote tulikuwa watulivu tofauti na siku nyingine. Hakukuwa na maneno mengi ya kushukuru wala mazungumzo ya mapenzi k**a nilivyotarajia. Kitu pekee nilichokuwa nakisikia ni sauti ya kiyoyozi cha gari na mapigo ya moyo wangu yaliyokuwa ya kawaida kuliko wakati mwingine wowote.

Ajabu ni kwamba, tangu lile jiwe la pete kupoteza rangi yake na kubaki pete ya kawaida ya shaba, nilihisi amani ambayo sikuwa nimewahi kuihisi kwa muda mrefu.

Tulipofika, mama yake Zuwena alitupokea huku akitokwa na machozi ya furaha. Baba yake naye alitoka nje taratibu, mwili wake ukiwa bado dhaifu lakini uso wake ukiwa mwepesi kuliko mara ya mwisho nilipomuona.

"Karibu mwanangu Clever," alisema huku akinishika mkono. "Mimi sina cha kukulipa. Umeturudishia heshima yetu."

Nilitabasamu tu. Kwa mara ya kwanza nilihisi k**a kuna kitu kilikuwa kinajengeka ndani yangu ambacho hakikuhitaji pesa.

Tulikaa kwa muda tukizungumza, kisha nikajiandaa kuondoka.
Zuwena alinisindikiza nje.

"Asante kwa kila kitu," alisema.
Nilitabasamu.

"Hakuna haja ya kunishukuru sana. Nadhani kila kitu kilitakiwa kutokea namna hii."

Zuwena alinitazama kwa muda mfupi halafu akasema.

"Clever… unaamini kweli kwamba kuna vitu vinatokea kwa sababu maalumu?"

Swali lake lilinifanya nitulie kidogo.
"Ndiyo. Naamini."
Hakujibu. Alitabasamu tu, lakini tabasamu lile lilikuwa tofauti. Halikuwa la furaha kabisa wala huzuni kabisa. Sikutumia muda mrefu, niliondoka.

Usiku ulipofika nilijitupa kitandani lakini usingizi haukuja mapema. Nilitoa mkono wangu nje ya shuka na kuitazama ile pete.

Haikuwa na jiwe tena.
Niliigeuza geuza mkononi.
Kabla sijalala, ghafla nilihisi kitu cha ajabu.

Pete ilianza kupata joto la kawaida tu… si moto… si maumivu… ila joto ambalo sikuwahi kulihisi.

Niliketi kitandani haraka.
Nikaitazama vizuri.
Palepale ambapo jiwe lilikuwa limepotea… kulikuwa na mstari mdogo wa maandishi ambao sikuwa nimeuwahi kuona.

Nilisogea karibu na mwanga.
Kwa shida nikasoma maneno yale.
"USIFIKIRI SAFARI IMEISHA."
Mwili mzima ulisisimka.
Niliisugua pete kwa nguvu nikidhani labda nimechoka au ninaota.
Lakini yale maandishi hayakutoweka.
Ghafla nikakumbuka maneno ya Mzee Ling’ande…

"Usimfahamu kwa haraka."
Nilikaa kimya kwa dakika kadhaa.
Asubuhi yake nilifanya uamuzi ambao sikuwahi kufikiria ningeurudia.
Nitarudi Lindi.

Lakini kabla hata sijaanza maandalizi ya safari, simu yangu iliingia ujumbe kutoka namba nisiyoifahamu.
Ujumne ulikuwa mfupi.

"Ukifika kwa Mzee Ling’ande… muulize kwanini hakukuambia ukweli wote."

Nilihisi damu ikiganda.
Namba ile haikuwa na jina.
Lakini mwisho wa ujumbe kulikuwa na herufi moja tu.

Z.

Usikose sehemu ya 10…

Karibu kwa maoni na ushauri.....

19/06/2026

SIKU MOJA UTAACHA KUJILAUMU

Ni kweli kwamba inaumiza sana,

Kubaki ukijiuliza k**a ungefanya zaidi,
ungeongea tofauti,
ungependa zaidi,
au ungevumilia kidogo labda mambo yangebaki k**a zamani.

Na kwa muda mrefu umekubali kubeba lawama ambazo si zako.

Ukafikiri ulipungukiwa.

Ukafikiri hukutosha.

Lakini leo nataka ukae kimya kidogo na ujisikilize.

Je, ni kweli uliyofanya ni kidogo?

Au ni kwamba ulifanya kila uliloweza kwa moyo uliokuwa nao kipindi hicho?

Kuna wakati tunachoka si kwa sababu hatukuwa na nguvu… bali kwa sababu tulikuwa tunapigania kitu peke yetu.

Inauma sana pale unapogundua ulikuwa unapambana kulinda kitu ambacho upande wa pili haukuwa unapambana kukibakiza.

Lakini hilo haliondoi uzuri wa moyo wako.

Naomba usiubadilishe moyo wako mzuri kwa sababu ya maumivu ya muda.

Usiache kuwa mtu wa kweli kwa sababu ulikutana na watu ambao hawakuwa wa kweli.

Najua sasa unaogopa kuamini.

Unaogopa kuzoea watu.

Unaogopa kujitoa tena.

Lakini usiufunge moyo wako milele.

Moyo haukuumbwa kuwa gereza.
Uliumbwa kupenda, kuamini, kuishi, kujifunza na kuendelea.

Na kuna jambo moja nataka ukumbuke siku ya leo…

K**a kuna mtu aliondoka wakati ulikuwa unampenda kwa dhati,
usiamini kuwa upendo wako haukuwa wa kutosha.

Wakati mwingine watu huondoka si kwa sababu hawakupata upendo…
bali kwa sababu hawakuwa tayari kuupokea.

Na siku moja…

Utakutana na amani ambayo
haitakulazimisha kulia ili uthibitike.

Na siku hiyo....

utajitazama kwenye kioo na kusema,
“Kumbe sikuwa nimevunjika… nilikuwa najijenga upya.”

18/06/2026

SIMULIZI; NAHITAJI NIMFAHAMU
MUANDISHI; ALLY H.

SEHEMU YA 08.

Saa mbili kamili asubuhi, korido za hospitali zilikuwa zimeanza kuchangamka. Nilikuwa nimekaa ndani ya ofisi ya Mkurugenzi wa Hospitali, Dr. Malise, mtu mwenye msimamo na asiyependa michezo na mali ya umma. Tulikuwa tushapitia nyaraka zote nilizozipata usiku kucha kwa msaada wa Saidi na Mzee Juma.

"Clever, k**a haya unayosema ni kweli, basi Dr. Frank amefanya makosa makubwa sana. Hatuwezi kuvumilia mtu anayetumia jina la hospitali yetu kudhulumu raia," Dr. Malise alisema huku akirekebisha miwani yake.

"Mkurugenzi, Zuwena anakuja ofisini kwa Frank sasa hivi. Naomba unisindikize huko, lakini tubaki nje ya mlango kwa dakika chache ili usikie mwenyewe jinsi anavyomshikilia huyu binti," nilimshauri.

Tulielekea ghorofa ya kwanza. Tukiwa tumesimama pembeni ya mlango wa ofisi ya Frank, tuliwasikia Zuwena na Frank wakiongea. Frank alikuwa na sauti ya dharau na kicheko cha kikebe.

"Zuwena, muda wa michezo umeisha. Karatasi hii hapa, saini kuwa unakubali kuhamia kwangu leo, na mimi nitaichana hii karatasi ya deni la baba yako mbele ya macho yako. Usijifanye unampenda yule kijana wa mtaani, hana lolote la kukusaidia," Frank alinguruma.

"Frank, lakini unajua sina hisia na wewe. Na unajua fika kuwa deni hili si la halali, hukulipa kiasi hicho," Zuwena alijibu kwa sauti iliyotetema lakini yenye ujasiri ambao sikuwahi kuuona kwake.

"Hahaha! Nani atakuamini? Mimi ndiye daktari mkuu hapa. Muhuri ni wa hospitali hii. Ukikataa, leo hii baba yako anafukuzwa wodini na ninafungua kesi ya madai. Utasota jela wewe na wazazi wako!"

Hapo ndipo Dr. Malise aliposhindwa kuvumilia. Alisukuma mlango kwa nguvu na kuingia ndani, mimi nikiwa nyuma yake.

Frank alishtuka kiasi cha kuangusha glasi ya maji aliyokuwa ameishika. Uso wake ulibadilika kutoka weusi na kuwa wa rangi ya kijivu. "Mmm.... Mkurugenzi? Karibu... nilikuwa nafanya mazungumzo ya faragha na nesi wangu."

"Mazungumzo ya faragha au ya kitapeli, Frank?" Dr. Malise aliuliza kwa sauti ya radi. "Nimesikia kila kitu. Tangu lini hospitali hii inaruhusu madaktari kutoa mikopo ya kinyonyaji kwa kutumia mihuri ya serikali?"

Frank alijaribu kujitetea, "Hapana, mzee... huyu binti aliniomba msaada, mimi..."

"Nyamaza!" Dr. Malise alimkatisha.

"Clever, nionyeshe ule mkataba.". Dr. Malise aliongea kwa msisitizo.

Niliutoa ule mkataba wa mkono niliouchukua kwa mama yake Zuwena. Dr. Malise aliutazama na kuukanyaga kwa hasira. "Frank, kuanzia sekunde hii, umesimamishwa kazi kupisha uchunguzi wa matumizi mabaya ya ofisi na utapeli. Na kuhusu hili deni, nitalifuta mimi mwenyewe kwasababu nimegundua matibabu ya mzee yalilipwa na mfuko wa ruzuku ya dharura, hukutoa hata senti yako!"

Zuwena alianguka na kupiga magoti huku akianza kulia na kutoa machozi ya furaha. Frank alijaribu kunitazama kwa chuki, akitamani kunivamia, lakini hakukuwa na nafasi ya kufanya hivyo.

Muda huo huo Frank alitolewa nje ya hospitali na walinzi mbele ya wafanyakazi wenzake. Sifa yake ilikuwa imepotea ndani ya dakika tano tu.

Baada ya fujo zile kutulia, mimi na Zuwena tulienda kutulia kwenye ile bustani ya hospitali. Wakati huo jua lilikuwa limechoza vizuri na kutoa mwanga ambao uliangaza nyuso zetu. Zuwena alinitazama, macho yake yakiwa bado yana unyevu, lakini safari hii yalikuwa yanang'aa kwa amani.

Nilijisogeza karibu naye. Pete yangu ilikuwa imetulia, ikitoa mwanga hafifu wa rangi ya waridi (pink) rangi ambayo sikuwahi kuiona. Haikuwa inatoa maumivu tena. Moyo wangu ulikuwa unapiga kwa utulivu wa ajabu, 'lub-dub, lub-dub', k**a wimbo wa taratibu.

"Clever... sijui nikupe nini. Umeniokoa mimi na familia yangu. Mimi sikuwa na kitu, nilikuwa mfungwa," alisema huku akishika mkono wangu.

"Zuwena, mimi pia sikuwa na kitu. Nilikuwa na pesa, lakini sikuwa na mtu anayenipenda kwa dhati bila kuangalia biashara zangu. Pete hii ilinileta kwako si kwa sababu wewe ni nesi, bali kwa sababu moyo wako ulikuwa unatafuta mtu wa kweli," nilijibu huku nikimtazama kwa macho yaliyojaa huba.

Kwa mara ya kwanza, Zuwena alinisogelea na kunikumbatia. Kitendo kile, kilinifanya nihisi ile pete ikilegea kwenye kidole changu. Nilipotazama, lile jiwe lilikuwa limepotea na kubaki pete ya kawaida ya shaba.

Niligundua kuwa kazi ya pete ya Mzee Ling’ande ilikuwa imeisha. Nimeshamfahamu mwanamke wa maisha yangu.

"Clever," Zuwena aliniita huku akinitazama machoni. "Sasa Frank hayupo, na deni limeisha. Naomba nikuulize kitu kimoja."

"Niambie, Zuwena."

"Ile pete yako... mbona kila tukikutana ilikuwa inabadilika rangi? Na mbona sasa hivi imetulia?"

Nilitabasamu. Nilijua siri hii itabaki kuwa yetu mimi na yeye milele. "Ni hadithi ndefu, Zuwena. Lakini neno moja unalotakiwa kujua ni kwamba, moyo wako ndio uliobadilisha rangi ya maisha yangu."

Tuliondoka hospitalini hapo tukiwa tumeshikana mikono, kuelekea kumuona mama yangu na baba yake Zuwena, tukijua kuwa safari yetu ya kweli ya mapenzi ndiyo kwanza inaanza.

Usikose sehemu inayofata.........

Karibu kwa maoni na ushauri.......

16/06/2026

Simulizi; NAHITAJI NIMFAHAMU
Muandishi; ALLY H.

SEHEMU YA 07.

Nilipokuwa ndani ya gari niliendelea kuifikiria ile rangi ya dhahabu iliyometa kwenye jiwe la pete, nilijiuliza maswali bila kupata majibu. Nilikumbuka maneno ya Mzee Ling’ande

"Ukiona rangi inabadilika nje ya utaratibu niliokupa, jua moyo wako unahitaji mwongozo wa ziada."

Sikurudi nyumbani. Badala yake, nilielekea upande wa pili wa mji wa Morogoro, eneo la Kihonda, kumtafuta mzee mmoja aliyeitwa Mzee Juma. Huyu alikuwa rafiki wa marehemu baba yangu na alikuwa mhasibu mkuu mstaafu wa serikali. K**a kuna mtu anayejua jinsi ya kufuatilia mikataba ya kinyonyaji na madeni ya kitapeli, basi ni yeye.

"Clever, mwanangu. Karibu," Mzee Juma alinisalimia huku akiniandalia kiti. "Unaonekana una jambo zito moyoni."

Nilirusha karata zangu zote mezani. Nilimuelezea kuhusu Zuwena, kuhusu Dr. Frank, na kuhusu lile deni la matibabu ya baba yake Zuwena ambalo Frank analitumia k**a pingu.

Mzee Juma alicheka kicheko cha busara.

"Kijana, katika ulimwengu wa sheria na fedha, hakuna deni lisilo na mwisho. K**a Frank alilipia matibabu, lazima kuna stakabadhi (receipts) na lazima kuna mkataba uliosainiwa. Shida ya watu wengi ni kuogopa majina makubwa k**a 'Daktari Mkuu'. Lakini daktari huyo huyo anaweza kuwa mwizi wa mali za umma."

Mzee Juma alinipa mbinu. "Nenda hospitalini, lakini usiende kwa Zuwena. Nenda idara ya uhasibu (accounts). Tafuta siri ya malipo ya mgonjwa anayeitwa mzee huyo, baba yake Zuwena. Ukigundua kuwa Frank hakulipa kwa pesa yake, bali alitumia bima ya hospitali au ruzuku ya serikali, basi Frank atakuwa amejichimbia kaburi mwenyewe."

Niliondoka kwa Mzee Juma nikiwa na nguvu mpya. Lakini kabla sijafika kwenye gari, simu yangu iliita.
Zuwena ndiye alikuwa akinipigia!, sauti yake ilidhihirisha hakuwa sawa, alikuwa akizungumza huku akilia.

"Clever... nisaidie. Frank amekuja nyumbani kwetu sasa hivi. Amesema anataka nimpe jibu la mwisho kuhusu kuhamia kwake kuanzia kesho, vinginevyo atawadai wazazi wangu pesa zote ndani ya masaa 24. Na amesema k**a sitakubali, atahakikisha baba haruhusiwi tena kupata matibabu ya kliniki hapa hospitalini."

Akili ilinituma nifike hapo nyumbani kwao na kumpasua Frank, lakini niliikumbuka ile rangi ya dhahabu iliyomaanisha hekima ilihitajika.

"Zuwena, usikubali wala usikatae. Mwambie akusubirie mpaka kesho asubuhi ufikirie. Nitumie 'location' ya nyumba yenu, nakuja sasa hivi." Niliongea kwa msisitizo.

Haikuchukua mda mrefu nilifika eneo la tukio. Niliegesha gari langu mbali kidogo, nikaona gari la Frank likiwa limepaki nje ya nyumba ya kina Zuwena. Baada ya k**a dakika 5, Frank alitoka huku akionekana na tabasamu la ushindi. Alipita na gari lake karibu na nilipokuwa, bila kuniona.

Nilisubiri Frank apotee, kisha nikashuka na kuelekea mlangoni. Zuwena alitoka nje, macho yake yakiwa yamevimba kwa kulia. Nilipata bahati ya kumshuhudia mama yake Zuwena ambaye alionekana mnyonge sana.

"Clever, kwanini umekuja? Frank anaweza kurudi muda wowote," Zuwena alisema kwa sauti ya kukata tamaa.

"Sikuja kuleta fujo, Zuwena. Nimekuja kuleta uhuru wenu," nilisema huku nikimtazama mama yake. "Mama, mimi naitwa Clever. Naomba nione nyaraka zozote mlizosaini na Dr. Frank kuhusu matibabu ya mzee."

Mama yake Zuwena aliingia ndani na kutoa bahasha iliyochakaa. Ndani yake kulikuwa na karatasi moja tu ya mkataba wa mikono. Nilipoisoma, nilicheka kwa dharau. Haikuwa mkataba wa kisheria, ulikuwa ni utapeli wa wazi! Frank aliandika kuwa amewakopesha shilingi milioni kumi na tano, wakati gharama halisi za operesheni ile niliyokuwa nimeichunguza hazikuzidi milioni tano.

Lakini kitu kimoja kilinistua. Chini ya ule mkataba, kulikuwa na muhuri wa hospitali ya mkoa. Frank alikuwa ametumia muhuri wa serikali kuhalalisha deni lake binafsi. Huu ulikuwa ni uhalifu wa kiuchumi!

Ghafla, pete yangu ilianza kutoa mlio mdogo wa 'beeeep', sauti ambayo sikuwahi kuisikia. Lile jiwe likabadilika na kuwa rangi ya bluu ya bahari tulivu na yenye amani. Nilihisi amani ya ajabu. Nilimshika Zuwena mikono yote miwili mbele ya mama yake.

"Zuwena, niamini. Kesho asubuhi, Frank atakuita ofisini kwake akitegemea ushindi. Nataka uende, lakini usiende peke yako. Utatengeneza mazingira ya yeye kukiri kuwa hili deni ni la kwake binafsi na si la hospitali."

"Lakini Clever, akigundua unanisaidia..."

"Hagundui. Maana kesho, mimi nitakuwa ndani ya hiyo ofisi kabla hata ninyi hamjafika."

Zuwena alinitazama kwa mshangao. Hakujua kuwa nilikuwa na marafiki kila mahali, kuanzia sokoni mpaka idara ya usalama.

Usiku ule, niliandaa mpango wa mwisho. Nilijua fika kuwa Frank ni mjanja, lakini hakujua kuwa anaumbuliwa na kijana anayetumia "macho ya moyo".

Kesho yake asubuhi, nilifika hospitalini saa kumi na mbili na nusu asubuhi, nikiwa nimevalia suti nadhifu, nimebeba mkoba wa ngozi. Nilielekea moja kwa moja ofisi ya mkurugenzi wa hospitali, ambaye alikuwa ni bosi wa Frank.

Je, Clever atafanikiwa kumuingiza Frank kwenye mtego?

Usikose sehemu ya 08...

Karibu kwa maoni na ushauri....

15/06/2026

Simulizi; NAHITAJI NIMFAHAMU
Muandishi; Ally H.

SEHEMU YA 06

Ujumbe ule wa vitisho uliniacha nikiwa na hasira iliyochanganyika na kiwewe. Nilijua fika kuwa Frank ana nguvu na ushawishi mkubwa pale mjini, lakini kitendo cha kunitishia maisha na biashara zangu kilichochea kitu fulani ndani ya damu yangu, ubishi wangu wa asili ulizinduka.

"K**a mzee wa Lindi hakunidanganya, basi Zuwena ndiye. Na k**a yeye ndiye, siwezi kumuacha mikononi mwa Frank," nilijisemea moyoni huku nikikunja ngumi.

Siku iliyofuata, niliamua kuanza na jambo moja ambalo niliona ni la muhimu. Nilimtafuta rafiki yangu mmoja aliyekuwa akifanya kazi ya usalama wa jamii, alikuwa akiitwa Saidi. Nilitaka anipe picha halisi ya Dr. Frank. Saidi alipokuja ofisini kwangu, alikuwa na habari ambazo zilinifanya nisisimke mwili kwa hasira.

"Clever, huyu daktari unayedeal naye ni mjanja sana. Kila mtu anajua Zuwena ni mchumba wake, lakini ukweli ni kwamba Frank hajawahi kuwa na nia ya kumuoa binti yule," Saidi alisema huku akishusha sauti.

"Anamtumia tu Zuwena k**a 'pambo' la kumpunguzia stress. Ana mwanamke mwingine wa hadhi yake kule Dar es Salaam ambaye mipango ya ndoa imepamba moto. Zuwena anashikiliwa hapa kwa sababu ya lile deni la matibabu ya baba yake. Frank anamfanya k**a mateka wa mapenzi."

Taarifa zile zilinitia uchungu kifuani. Niligundua kuwa Zuwena hapendwi, bali anadhulumiwa utu wake. Nilishindwa kuvumilia, nikaamua kwenda hospitali, si k**a mgonjwa, bali k**a mtu anayetafuta ukweli.

Nilimkuta Zuwena akiwa amekaa peke yake kwenye benchi la nje, akitazama mbali kwa huzuni. Nilipokaribia, pete yangu ilianza 'pum! pum! pum!' kwa kasi ya ajabu. Rangi nyekundu ilianza kusambaa k**a moto kwenye lile jiwe.

"Zuwena," nilimwita kwa sauti ya chini.

Alishtuka na kusimama, uso wake ukijaa hofu. "Clever! Kwanini umerudi?, unatatizo gani lakini wewe?, si nimekwambia usiwe unakuja hapa kunifatilia, na k**a haitoshi, je haukupata onyo kutoka kwa frank?"

"Samahani!, nilipata ujumbe ambao unauita onyo katika simu yangu, na ndio maana nimekuja. Zuwena, nimegundua kila kitu. Najua Frank hajakuchagua k**a mke, bali anakutumia k**a rehani kwa sababu ya deni. Kwanini unakubali kuishi kwenye jela hii?" nilisema nikiwa nimesimama hatua chache kutoka kwake.

Zuwena alishusha pumzi ndefu, machozi yakimlengalenga.

"Clever, hujui unachokisema. Duniani hapa fadhila hulipwa kwa gharama kubwa. Frank alimwokoa baba yangu wakati hakuna daktari aliyekuwa tayari kugusa jeraha lake bila pesa. Leo hii nitalipaje deni hilo ikiwa sina hata thumni? Naweza kumchukia Frank, lakini siwezi kumtelekeza baba yangu."

"Lakini anakudanganya, Zuwena! Ana maisha mengine kule Dar, na hapa anakuweka k**a pambo tu, kiufupi Frank sio binadamu, hauthamini utu wako, anakutumia kisha baadae akuache," nilizidi kusisitiza, huku nikisogea karibu zaidi. Kwa sekunde ile, nilimshika mkono wake. Pete iliwaka kiasi cha kuonekana hata kwa macho ya kawaida. Nilihisi mitetemo ya moyo wake ikikutana na yangu, kuna namna nilijihisi k**a nipo katika ulimwengu ambao haufanani na dunia tunayoishi, ulimwengu ambao haulezeki, ni moyo wangu tu ndo ulibaki na siri hiyo.

Zuwena hakutoa mkono wake. Kwa mara ya kwanza, alinitazama kwa macho yaliyojaa kiu ya msaada.

"Hata k**a unachosema ni kweli... Frank ni daktari mkuu hapa. Anaweza kuhakikisha biashara zako zote Morogoro zinafungwa ndani ya usiku mmoja. Ana watu kila mahali, Clever. Usipoteze maisha yako kwa ajili ya mimi niliyekwisha haribikiwa."

Wakati anasema maneno hayo, mmoja wa walinzi wa hospitali alitupita na kututazama kwa jicho la shaka. Zuwena alishtuka na kuondoa mkono wake kwa haraka.

"Ondoka sasa hivi, Clever. Tafadhali. Usifanye hali iwe mbaya zaidi," alisema huku akigeuka na kukimbia kuelekea wodini.

Nilibaki nimesimama, nikiwa nimeshikilia kifua changu kilichokuwa kikidunda. Niligundua kuwa Frank hamfuatilii Zuwena kwa mapenzi, bali anafuatilia mali yake isitoroke. Nikiwa narudi kwenye gari langu, nilihisi kioo cha ofisi ya Dr. Frank iliyoko ghorofa ya kwanza kikifunguliwa.

Nilipotazama juu, nilimuona Frank akiwa amesimama, akiwa ameshika glasi ya kinywaji, akinitazama kwa namna isiyoeleweka, sura yake haikuonesha dalili ya wema. Macho yake ni k**a yalikuwa yakiniambia kuwa. "Unachokitafuta utakipata kijana."

Kwenye akili yangu niliwaza kuwa, vita ile nilihitaji kuipigana kwa akili na sio ngumi. Lakini swali likabaki, nitaanzaje kumtoa Zuwena kwenye lile deni la mamilioni?

Niliingia kwenye gari, nikaitazama ile pete. Ghafla, nikaona rangi ya kijani inaanza kubadilika na kuwa ya dhahabu kwa sekunde chache, kisha ikarudi kijani. Sikuwahi kuona mabadiliko hayo tangu nivae. Je, Mzee Ling'ande alikuwa ananipa ishara nyingine?, nilijiuliza lakini sikupata majibu.

Niliwasha gari na kuelekea sehemu moja ambayo nilijua nitapata msaada wa kumshuhulikia daktari tapeli, Doctor Frank.......

Usikose sehemu ya 07...

Karibu kwa maoni na ushauri........

Want your business to be the top-listed Gym/sports Facility in Kilindoni?

Click here to claim your Sponsored Listing.

Location

Telephone

Website

Address

Kilindoni